Tuesday 30 May 2017

UZURI WA MKALAMA

Mzee Wilfred Mlundi na Mbizi Kitundu ambao mpaka sasa wapo katika kijiji cha Mkalama  walifanya kazi wakati wa enzi za utawala wa Ujerumani waliofika nchini Tanzania baada ya Vita kuu ya kwanza ya dunia.

Hiki ni kisima cha maji ambacho kipo katikati ya jiwe kubwa katika kijiji cha Isanzu . Maji haya hayajawahi kuisha hata yakitumiwa kiasi gani.

Unyayo wa mtu wa kale kama unavyoonekana pichani ukiwa katikati ya jiwe katika kijiji cha Isanzu.

Pichani hapo kwenye uwazi ndipo palipokuwa pakitumika kwa ajili ya mikutano mbalimbali na serikali ya wakoloni wa Kijerumani.

Haya ndo yalikuwa makazi, Ofisi na Mahakama ya Serikali ya wakoloni wa Kijerumani wakati wa Utawala wao yaliyopo katika kijiji cha Mkalama. 




Neno Mkalama linatokana na neno la  lugha ya asili ya kabila la wanyiramba ambalo lilizaliwa baada ya mti mkubwa sana kuliko yote kwenye kijiji hicho kuonekana kulalia upande mmoja ambapo kitendo hicho ndio huitwa “kukalama”. Baadaye mti huo maarufu ulipewa jina la “ Mkalama” ambalo lilienea sana na hatimaye kijiji chote kupewa jina hilo.

Pengine unaweza kudhani uzuri wa Mkalama unaishia hapo La hasha! Wakati  wa uasisi wake, Kijiji cha Mkalama kilikuwa chini ya Wilaya ya Iramba ambayo ni moja ya Wilaya zilizopo katika Mkoa wa Singida lakini baada ya kutanuka kwa wigo wa upatikanaji wa huduma za Msingi, serikali iliamua kuigawa Wilaya ya Iramba na hatimaye kupatikana Wilaya nyingine ambayo kwa heshima na uzuri wa yanayopatikana katika kijiji cha Mkalama serikali iliamua kuipa Wilaya hiyo mpya jina la Mkalama.

Labda msomaji yoyote wa Makala hii anaweza kujiuliza ni mambo gani yaliyonisukuma kuelezea uzuri wa Wilaya hii, naomba nichukue fursa hii kukudokeza japo kwa uchache yanayopatikana katika Wilaya hii.

Hapo hapo katika kijiji cha Mkalama ndipo yalipokuwa makazi ya kudumu ya Wajerumani walipofika Tanganyika na kwa Mujibu wa Mzee Mbizi Kitundu na Wilfred Mulundi ambao walifanya kazi wakati wa Utawala wa wajerumani hao, Wajerumi walikuwa wakitumia sana usafiri wa farasi ambao waliendeshwa na wafanyakazi wa kiafrika kwa ajili ya kupokea na kusindikiza wageni hao.

Kivutio kikubwa hapo ni wazee hao ambao mpaka sasa hawajui wana umri wa miaka mingapi lakini kutokana na ukweli kuwa wajerumani waliondoka kabisa Tanganyika baada ya Vita kuu ya Kwanza ya Dunia,  wazee hao wanakadiriwa kuwa na zaidi ya miaka 120 na hata unapozungumza nao ni lazima ukae kando yao ndipo uweze kusikia wanachozungumza na hawazungumzi lugha yoyote zaidi ya kijerumani na kinyiramba.

Ushahidi juu ya uwepo wa wajerumani waliofika katika Wilaya ya Mkalama unapatikana katika kijiji cha Mkalama kupitia magofu makubwa ambayo waliyatumia kwa makazi, Ofisi na mahakama.

Si mapango ya wajerumani pekee yanayoifanya Mkalama kuwa Mji uliojaa wingi wa vivutio kwani Uwepo wa mapango makubwa katika kijiji cha Isanzu ni moja ya mambo ambayo huwezi kukubali kuyakosa.

Ukiacha uzuri wa mapango hayo, mambo ya kuzingatia kabla ya kuingia kwenye mapango hayo ni moja ya mambo  yanavutia zaidi, Naomba nichukue fursa hii kukujuza mambo hayo.

Kabla ya hujaingia kwenye msitu huo ni lazima uhakikishe hauna kitu chochote chenye rangi nyekundu kwa sababu rangi hiyo huwa inachukuliwa kama ni rangi ya kafara na hivyo kumfanya yoyote anayeonekana na vazi hilo kuwa kama mtu mwenye mkosi.

Ndani ya mapango hayo  kuna mti ambao mnyama yoyote ambaye anaweza kuchinjwa huwa analala tu bila tatizo taari kwa kuchinjwa bila kushikwa na mtu wala kufungwa Kamba na jambo hilo linamhusu mnyama yoyote bila kujali umbo alilonalo au aina ya ukali alionao.

Pia kuna ngoma kubwa zenye urefu usiopungua mita saba ambazo zilikuwa zinatumiwa na watu walioishi kwenye mapango hayo hali inayoashiria kuwa Watu wa kale walikuwa warefu sana kiasi cha kumudu kupiga ngoma hizo huku wakiwa wamesimama.

Huku ukistaajabu hayo unapaswa kujua kuwa Kijiji cha Isanzu ndipo sehemu ambapo utaziona nyayo za watu wa kale na cha kushangaza zaidi nyayo hizo zipo juu ya mawe hali inayozua maswali mpaka leo juu ya kipimo cha uzito waliokuwa nao watu wa kale.

Mkalama imezungukwa na milima ambayo tofauti na milima inayopatikana sehemu nyingine kwani milima hii ndani yake kuna mapango makubwa yenye michoro ya aina mbalimbali lakini cha kufurahisha zaidi ni uwepo wa viumbe ambao mpaka sasa hawajajulikana ni viumbe wa aina gani lakini mara kwa mara muda wa jioni watu wanaoishi karibu na milima hiyo wamekuwa wakisikia ngoma na sauti mbalimbali zikiimba nyimbo za asili na mara nyingi
kwa mujibu wa wazee wakongwe wanaoishi maeneo hayo wanasema hao ni mabaki ya vizazi vya watu wa kale kabisa ambao mpaka leo wanaishi katika milima hiyo huku chakula chao kikubwa kikiwa ni matunda ya porini na wanyama pori.

Kwa leo naomba niishie hapa, Mungu akipenda tutaendelea na Makala haii ili uzidi kuufahamu utamu na uzuri wa Wilaya ya Mkalama.

Maoni au Ushauri: 0655949391.


No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA