Friday 23 November 2018

Kampeni hii ifanyike katika kata zote-DC

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka akihutubia umati wa watu waliojitokeza kwenye sherehe za uzinduzi wa kampeni ya Furaha yangu zilizofanyika katika kijiji cha Nkalakala leo.

Muuguzi wa zahanati ya Nduguti Bi. Josephine Makanyaga akitoa maelezo juu ya namna zoezi la damu salama linavyotekelezwa mbele ya mkuu wa wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka (kushoto) wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Furaha yangu"uliofanyika katika kijiji cha Nkalakala leo.

Kikundi cha Ngoma kutoka kijiji cha Nkalakala  kikitumbuiza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya "Furaha yangu" leo katika kijiji cha Nkalakala.



“Ninaagiza kampeni hii ifanyike katika kata nyingine zote 16 zilizobakia za Wilaya yaMkalama”

Hilo ni agizo lililotolewa na Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka wakati wa uzinduzi wa kampeni ya upimaji wa hiyari wa  virusi vya ukimwi iliyopewa jina la “Furaha Yangu” uliofanyika leo katika kijiji cha Nkalakala ambapo zaidi ya watu 250 walijitokeza kupima.

Katika hotuba yake Mhe. Masaka alimshukuru Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kwa kuzindua kampeni hiyo kitaifa yenye lengo la kuhamasisha wananchi hasa wanaume kujitokeza kwa wingi katika vituo vya afya kupima kwa hiyari virusi vya ukimwi.

“Kwa Wilaya ya Mkalama suala la kupima afya sio jipya kwetu kwa sababu nimeshuhudia watu wengi sana wakijitokeza kupima afya zao kipindi cha mkesha wa Mwenge na sherehe nyingine huku vipimo mbalimbali vikifanyika ikiwemo shinikizo la damu, Malaria na HIV/VVU” aliongeza Mhe. Masaka.

Mhe. Masaka aliwasisitiza wananchi wote wa Mkalama kuchukua tahadhari kwa kujikinga na kuwakinga wengine dhidi ya maambukizi ya Ukimwi ili kuweza kupunguza kasi ya maambukizi ya ugonjwa huo ambayo kwa mkoa wa Singida imeonekana kukua kwa asilimia 0.3 kutoka asilimia 3.3 ya mwaka 2011/2012 hadi asilimia 3.6 ya mwaka 2016/2017.

“Lakini pia ninaomba wananchi msipuuze pindi mnapobanwa na vikohozi visivyoisha kwa sababu huenda ikawa ni dalili ya ugonjwa wa Kifua kikuu kwa hiyo usijikaushe ewe dada na kaka nendeni mkapime na bahati nzuri Wilaya yetu imepata wahisani wa kusaidia mapambano dhidi ya virusi vya Ukimwi na TB  na kampeni hizi ni msaada mkubwa kwa afya zetu” Aliongeza Mhe. Masaka.

Mhe. Masaka alihitimisha hotuba yake kwa kuwahimiza wananchi wote kuwashawishi vijana na watoto wao wasome kwa bidii masomo ya sayansi ili waweze kupata nafasi za kusomea uuguzi, ukunga, maabara, udaktari na kozi nyingine za afya kwa sababu wasipofanya hivyo watakuwa na majengo mazuri ya zahanati, vituo vya afya na hospitali lakini hakutakuwa na wataalam wa kuendesha vituo hivyo.

Kampeni ya “Furaha Yangu” ilizinduliwa kitaifa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa mnamo tarehe 16 mwezi juni mwaka huu makao makuu ya nchi jijini Dodoma.


No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA