Tuesday 30 May 2017

Ni jukumu letu sote kuwalea "wakoma"- Masaka

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Nkungi wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Mhandisi Jackson Masaka wakati wa kuwagawia msaada wa chakula na vitu mbalimbali waathirika wa ugonjwa wa Ukoma maarufu kama Wakoma mwishoni mwa wiki iliyopita.



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga ametoa msaada wa chakula na vitu mbalimbali vyenye thamani ya zaidi ya Shilingi laki sita kwa wananchi wa kijiji cha Nkungi ambao waliathiriwa na ugonjwa wa Ukoma maarufu kama Wakoma.

Akizungumza kabla ya kukabidhi vifaa hivyo, Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Mhandisi Jackson Masaka amesema kuwa hivi sasa Wilaya inafanya utaratibu wa kuanza kuwahudumia wakoma hao badala ya kusubiri misaada kutoka kwa wahisani mbalimbali.

“Misaada inachukua muda mrefu kufika na ikifika inakuwa ni michache hali inayozidi kuwapa wakati Mgumu waathirika hawa kwa sababu wanahitaji uangalizi wa hali ya juu” Alisema Masaka.

Mhe: Masaka amewapongeza wadau wa shirika la African Smile kwa kujitolea kujenga nyumba za waathirika hao na kutoa rai kwa vijana na wananchi wa kijiji hicho kuendelea kujitolea kuwasaidia katika kuboresha makazi ya waathirika hao.

Aliongeza kuwa shirika la FCC liliwasilisha barua ofisini kwake na kuwaandikia barua ya kupewa msamaha wa kodi ili waweze kupitisha chakula cha waathirika hao ambacho hutolewa na watu wa Marekani hivyo muda wowote kuanzia sasa chakula kitakuwa kimeshafika katika kambi hizo za Wakoma.

“Lakini kwa sababu mimi ni kiongozi wa Wilaya ninaagiza Mkurugenzi uwaandikie watendaji wa kata ili kila kata itoe kiasi cha gunia moja kwa ajili ya kuzisaidia kambi hizi na naomba nipate taarifa ya utekelezaji juu ya hili” Aliagiza na kumalizia Masaka.

                

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA