Tuesday 5 June 2018

MKALAMA yafanya DCC ya kwanza leo





Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka akihutubia wakati wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) kilichofanyika leo katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga akizungumza machache kabla ya kumkaribisha Mgeni rasmi  wakati wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) kilichofanyika leo katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo.

Wajumbe mbalimbali waliojitokeza akihutubia wakati wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) kilichofanyika leo katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo.




Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka leo ameongoza kikao cha kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC)  ambapo katika hotuba yake ametoa maelekezo mbalimbali kwa wadau na idara mbalimbali zilizopo Wilayani Mkalama.

Kikao hicho mbali na kuhusisha baraza lote la Madiwani, pia kilihusisha taasisi mbalimbali zinazoendesha shughuli zake Wilayni Mkalama, Watendaji wote wa kata, wawakilishi wa taasisi za dini na wawakilishi wa vikundi mbalimbali vya ujasiriamali.

Mhe. Masaka aliwataka wananchi na viongozi kutambua umuhimu wa wingi wa fedha zinazotolewa na serikali katika kuhudumia Eimu nchini kwa kuhimiza watoto kwenda shule, walimu kufanya kazi pindi wawapo shuleni na wazazi kuonesha mwamko wakati wa kuchangia huduma mbalimbali za uboreshaji wa Elimu za watoto wao.

“Jambo la pili nitumie fursa hii kuhimiza wakulima wote walime mazao ya mkakati ambapo kwa Wilaya yetu mazao hayo ni pamba, korosho, alizeti na Vitunguu” Aliongeza Mhe. Masaka.

Mhe. Masaka alisisitiza kuwa ili kilimo cha Mkakati kiweze kuwa na tija ni lazima wakulima watumie mbegu bora, wapande mazao yao kwa vipimo sahihi na watumie vipimo stahili katika uwekaji wa dawa za kuua wadudu wanaoathiri mazao hayo.

“Mawakala wa huduma za Misitu nchini (TFS) na idara ya Maliasili ni lazima waonekane wapo badala ya kuziachia serikali za vijiji  kesi za uvamizi wa maeneo ya misitu ingawa pia vijiji vyote vinapaswa kulinda maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya misitu” Aliongeza Mhe. Masaka.

Mhe. Masaka alitumia fursa hiyo kusisitiza wananchi wajenge viwanda vidogo kama viwanda vya kukamua mafuta ya Alizeti na kuagiza kila mtu awaunge mkono wenye viwanda hivyo ili wafanikiwe na hatimaye waweze kufungua viwanda vikubwa.

“Sio Afisa afya anaenda kukagua kiwanda na kukuta mazingira yasiyoridhisha lakini badala ya kushauri namna ya kuboresha mazingira hayo anaamua kuchukua uamuzi wa kukifunga kiwanda hicho” Alisisitiza Mhe. Masaka.

Katika  hotuba yake Mhe. Masaka pia  alizitaka taasisi zote zinazofanya shughuli zake Wilayani Mkalama kuwa na mipango yenye mwelekeo mmoja ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma zote za msingi kwa wakati badala ya huduma moja kusubiri uwepo wa huduma nyingine.

“Sio Tarura wanajenga barabara Kinyambuli, Halmashauri inaenda kujenga kituo cha Afya Gumanga, Tanesco wanapeleka umeme Kinyangiri na Idara ya Maji wanapeleka maji Ibaga, hapo mtakuwa hamjamsaidia mwananchi kwa sababu hata mkimpelekea kituo cha Afya kizuri, kama hakuna barabara nzuri kufika kwenye kituo hicho au umeme wa kutumia kituoni hapo itakuwa ni kazi bure” Alisema Mhe. Masaka.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Masaka aliwaomba wananchi na taasisi za dini zilizopo wilayani Mkalama kuisaidia serikali kwa kutoa maeneo ambayo hawayatumii ili yatumike katika shughuli za Maendeleo.

“Msiishie tu kumiliki maeneo hayo bila kuyaendeleza kwa kufanya shughuli za Maendeleo hivyo kama ni kilimo limeni, kama ni viwanda wekeni viwanda na kama mlipanga kuweka taasisi za Elimu wekeni taasisi hizo” Alimalizia Mhe. Masaka.




No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA