Friday 18 May 2018

Elimu Mkalama ibadilike kwa vitendo-Nchimbi

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Daktari Rehema Nchimbi akisoma hotuba yake wakati wa kufunga maandhimisho ya Juma la Elimu, tukio lililofanyika leo mchana katika Viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama akiwasalimia wananchi wote waliofika kwenye kilele cha maadhimisho ya Juma la Elimu,tukio lililofanyika leo mchana katika Viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama. 

Afisa Elimu wa Mkoa wa Singida Bi. Nelasi Mulungu akisoma jumla ya mambo mbalimbali yaliyoainishwa na timu ya wataalam wa  Wilaya ya Mkalama kwa kushirikiana na Mtandao wa Elimu Tanzania na wadau wengine mbalimbali wa Elimu kwenye kilele cha maadhimisho ya Juma la Elimu,tukio lililofanyika leo mchana katika Viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama. 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Daktari Rehema Nchimbi akiwa ameshikana mikono na  wageni waalikwa na wanafunzi wa shule ya Msingi Mbigigi kama ishara ya kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya Juma la Elimu duniani isemayo "Uwajibikaji wa pamoja kwa Elimu bora kwa wote"


“Elimu ni moyo wa uhakika na hakikisho la uhai wa maendeleo endelevu ya familia, jamii na Taifa kwa ujumla”

Hayo ni maneno yaliyotamkwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Daktari Rehema Nchimbi ambaye alikuwa Mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya Juma la Elimu tukio lililofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.

Mhe. Nchimbi ambaye alimwakilisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) Mhe. Selemani Jafo, alitumia fursa hiyo kuwashukuru wadau wote wa elimu chini ya mwamvuli wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TenMet) ambapo aliwataka watumie maadhimisho ya mwaka ujao kutoa majibu ya tathmini ya utekelezaji wa changamoto zote walizoziona katika Wilaya za Nanyumbu na Mkalama.

“Haiwezekani kila mwaka muwe mnazungumzia changamoto za aina moja hivyo ni lazima muweke mpango mzuri wa kufanya ufuatiliaji wa karibu wa utekelezaji wa changamoto zote mlizoziainisha” Alisisitiza Mhe. Nchimbi.

Mhe. Nchimbi aliushukuru uongozi na wananchi wa Mkalama kwa ujumla kwa kuahidi kubadilisha matokeo waliyoyapata mwaka jana ambapo aliwasisitiza wajikite zaidi kwenye mabadiliko ya vitendo badala ya maneno.

Kabla ya kutangaza kufunga maadhimisho ya juma la Elimu kwa mwaka huu, Mhe. Nchimbi aliendesha harambee ya kuchangia elimu Wilayani hapa ambapo jumla ya shillingi 600,000 zilipatikana.

Awali akizungumza maneno machache kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka alisema kuwa TenMet waliamini Mkalama bado ipo hai ndio maana walifika kuisaidia kuainisha sababu mbalimbali zilizosababisha kutokuwa na matokeo mazuri ambapo aliwaahidi kuwa Wilaya yake haitofanya vibaya tena.

Wakati huo huo Mhe. Masaka alitumia fursa hiyo kuwatakia kila la kheri waislam wote wa Wilaya ya Mkalama katika Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ambapo aliwataka wafanyabiashara wote Wilayani hapa kutopandisha bei za vyakula ambavyo hutumiwa kama futari na daku  katika kipindi hiki.

“Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya itafuatilia kwa karibu sana utekelezaji wa agizo hili na atakayekiuka hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake” Aliongeza Mhe. Masaka.




No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA