Thursday 3 August 2017

Achia shoka kamata mzinga- Nchimbi




Mgeni rasmi wa ufunguzi wa Maonesho ya NaneNane kwa kanda ya kati Mhe: Daktari Rehema Nchimbi akifuatilia burudani muda mfupi baada ya kufika katika eneo la Sherehe.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe: Jordan Rugimbana akizungumza machache muda mfupi kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi wa Ufunguzi wa Maonesho ya 21 ya NaneNane kwa kanda ya kati Dodoma.


Mgeni rasmi wa ufunguzi wa Maonesho ya 21 ya  NaneNane kwa kanda ya kati Mhe: Daktari Rehema Nchimbi akitoa hotuba ya Ufunguzi katika Viwanja vya Maonesho ya NaneNane vilivyopo Eneo la Nzuguni Mkoani Dodoma..



Maadhimisho ya 21 ya Sikukuu ya Wakulima na Wafugaji maarufu kama NANENANE yamefunguliwa rasmi leo kwa kanda ya kati inayojumuisha mikoa ya Singida na Dodoma.

Mgeni rasmi katika Ufunguzi huo alikuwa ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Daktari Rehema Nchimbi ambaye alitumia muda usipungua dakika 45 kusisitiza umuhimu wa kuwekeza katika kilimo na ufugaji wenye  tija ili kuendana na falsafa ya serikali ya awamu ya Tano nayohimiza zaidi Uchumi wa Viwanda.

Mhe: Nchimbi amesema kuwa ni vizuri maadhimisho ya Mwaka huu yakaonesha mabadiliko chanya kwa washiriki waliojitokeza katika kuonesha bidhaa mbalimbali na wale waliofika kwa ajili ya kununua au kupata maelezo ya matumizi ya bidhaa hizo.

“ Nimepita kwenye banda la Jeshi la Magereza na kuona bidhaa nyingi sana zilizotengenezwa na Ngozi na wamenihakikishia kuwa kiwanda chao kina uwezo wa kununua ngozi yote inayopatikana katika Mikoa ya Singida na Dodoma hivyo ni vizuri tutumie hiyo kama fursa” Aliongeza Mhe: Nchimbi.

Mhe: Nchimbi ameliomba Jeshi la Magereza na wawekezaji wote wa ndani nan je ya Nchi wafike kuwekeza katika mikoa ya Singida na Dodoma na kwa kushirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma watahakikisha wanatengeneza mazingira rafiki kwa kila atakayekuwa tayari kuwekeza katika Mikoa hiyo.

“Kila siku huwa nasisitiza Mikoa ya Singida na Dodoma haina ukame na ndio maana hivi sasa tunataka kuanzisha mpango maalum wa kilimo cha umwagiliaji kwa sababu watafiti wameshatuhakikishia mikoa hii ina kiwango kikubwa sana cha maji ardhini tena yapo karibu sana na uso wa ardhi” Alisisitiza Mhe: Nchimbi.

Katika hatua nyingine Mhe: Nchimbi amewataka wananchi wa Mikoa ya Singida na Dodoma kuacha kabisa kukata miti kwa kisingizio cha kujikwamua kiuchumi kwa sababu kuna njia nyingi sana za kuondokana na hilo badala ya kuharibu misitu.

“Kule Singida nimeanzisha kampeni inayojulikana kama ‘ACHIA SHOKA, KAMATA MZINGA’ ambayo inampa mwananchi nafasi ya kuamua kuacha kukata mti na badala yake anafuga nyuki jambo linalomsaidia kujikwamua kiuchumi kwa muda mrefu zaidi kwa sababu unaweza kuukata mara moja tu lakini mzinga unaweza kuutundika mara nyingi kadri uwezavyo” Alisema Mhe: Nchimbi


Mhe: Nchimbi alimalizia hotuba yake kwa kuwasisitiza maafisa kilimo kupeleka kalenda za kilimo katika ngazi zote kuanzia ngazi ya kijiji ili iwe rahisi kwa Mkulima kujua aina ya mazao anayoweza kulima kwa Mwaka husika badala ya kumsubiri Mkulima apate madhara kwanza  ndipo aje apewe elimu ya mazao aliyotakiwa kulima kwa mwaka husika. 

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA