Friday 3 March 2017

KILA HALMASHAURI ITENGE BAJETI YA ZOEZI LA MADAKTARI BINGWA- NCHIMBI

PICHA MBALIMBALI ZIKIMUONESHA MKUU WA MKOA WA SINGIDA MHE: REHEMA NCHIMBI AKIWA AMEAMBATANA NA VIONGOZI MBALIMBALI WA MKOA NA WILAYA KATIKA ZIARA YAKE WILAYANI MKALAMA JANA.























Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi jana alifanya ziara Wilayani Mkalama ambapo alitembelea na kukagua miradi mbalimbali na kuzindua zoezi la madaktari bingwa linaloendelea katika hospitali ya Iambi.

Mara baada ya kufika katika hospitali ya Iambi, Mganga Mkuu wa Mkoa Dokta John Mwombeki alimsomea Mhe: Nchimbi  taarifa fupi ya zoezi hilo na jinsi lilivyofanyika katika Mkoa wa Singida ambapo taarifa hiyo ilieleza namna zoezi hilo lilivyofanyika kwa mafanikio huku likitarajiwa kuhitimishwa katika Wilaya ya Mkalama.

“Mpaka sasa jumla ya watu 675 wameonwa na madaktari bingwa na 71 kati yao wamefanyiwa upasuaji” Alisema Mwombeki.

Akizungumza mara baada ya kusomewa taarifa, Mhe: Nchimbi alimpongeza Mganga Mkuu wa Mkoa na timu yake kwa kufanikisha kufanyika kwa zoezi hilo ambapo alizitaka Halmashauri zote Mkoani Singida kuangalia namna ya kupata shilingi Milioni 18 kila Mwaka kwa ajili ya huduma za madaktari bingwa.

“Halmashauri zisisubiri kufuatwa na Mkoa kwa ajili ya zoezi hili bali ziandae ratiba na kuziwasilisha Mkoani ili zoezi hili liwe endelevu” Alisema Mhe: Nchimbi.

Aliongeza kuwa utengenezwe mfuko maalum kwa ajili ya zoezi hilo ili pesa inayopatikana katika mazoezi ya madaktari bingwa iwekwe humo kwa ajili ya kuhakikisha zoezi hilo linakuwa endelevu.

Kabla ya kuzindua zoezi la Madaktari bingwa, Mhe: Nchimbi alitembelea Chuo cha Maendeleo ya Jamii kilichopo katika kata ya Gumanga ambapo aliiagiza halmashauri ya Wilaya ya Mkalama iandae taarifa ya miaka mitano ya chuo hicho.

“Halmashauri ni lazima ikichukue chuo hiki na ihakikishe kinapata wanafunzi wa kutosha na viongozi wa Chuo ni lazima wabadilike na kutoa mapendekezo mazuri ya uendelezaji wa Chuo hiki”. Alisema Mhe: Nchimbi.

Alisema kuwa Mkoa na Halmashauri watumie chuo hicho kama sehemu ya mafunzo kwa watendaji wa kada zote na kisigeuzwe shule ya  kidato cha tano kama ilivyopendekezwa  bali halmashauri itafute mahali pengine na kuhakikisha inakuwa na shule ya ngazi ya kidato cha tano mwaka huu.

Alihitimisha kwa kuziagiza halmashauri zote Mkoani Singida kununua camera na vifaa vingine vya kisasa vitakavyowawezesha maafisa habari kufanya kazi zao kwa ufanisi badala ya kuwaacha wataalam hao kuendelea kutumia vyombo binafsi.

“Haiwezekani hawa wataalam wa serikali kuendelea kutumia vyombo binafsi, vyombo vina “filosofia” zao , tuwe na matukio yetu tuyaandae na kuyatangaza kwa sababu moja ya vitu vikubwa vinavyochagiza maendeleo ni kupata taarifa au habari” Alimalizia Mhe” Nchimbi.



No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA