Thursday 5 May 2016

MKALAMA KUONDOKANA NA UHABA WA MAJI

Tenki la kuhifadhia maji ya mradi wa Gumanga ambalo lina uwezo wa kuhifadhi lita elfu 90 za maji ambazo zitahudumia watu wote wa kata ya Gumanga. Mradi huu unasubiri jenereta tu uanze kufanya kazi.

Picha kubwa ni kibanda ambacho  jenereta la kusukuma maji ya mradi wa Gumanga litahifadhiwa na picha ndogo ni kisima ambacho kinatarajiwa kuzalisha maji hayo ambacho kina uwezo wa kuzalisha lita 2700 kwa saa.

Tenki la mradi wa maji wa Nyahaa ambalo lipo katika hatua za mwisho za ujenzi wake. Tenki hili lina uwezo wa kuzalisha lita 45,000 ambazo zitaweza kuhudumia wakazi wote wa kijiji cha Pambala.

kisima kitakachozalisha maji ya mradi wa Nyahaa ambapo kipo katika hatua za mwisho kukamilika.

Kibanda ambacho kitahifadhi jenereta ya kusukuma maji ya mradi wa Nyahaa kikiwa katika hatua za mwisho kukamilika.

Tenki kubwa la mradi wa maji wa Nyahaa ambalo lina uwezo wa kuhifadhi lita 135000 likiwa katika hatua ya mwisho kukamilika. Tenki hili litakuwa na uwezo wa kuhudumia wakazi wote wa kijiji cha Nyahaa na maeneo ya karibu ya Mkoa wa Simiyu.

Muonekano wa tenki hilo kwa ndani, hapa mafundi wakiendelea na kazi ya kuhakikisha linakamilika kwa wakati.

Mhandisi wa maji wa Wilaya ya Mkalama, Heke Bulugu (kushoto) akitoa maelezo na ufafanuzi wa mradi wa Nyahaa mbele ya Mwenyekiti wa kamati ya maendeleo ya huduma za jamii, Bi. Mariam Kahola na ujumbe uliotoka halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.

Tenki la mradi wa maji wa Iguguno ambao hapo awali ulikuwa ukitoa huduma upande mmoja tu wa kata hiyo kabla ya kusitishwa na kufanyiwa marekebisho ili uhudumie wakazi wote wa kata hiyo.

Tenki la mradi mkubwa wa Maji wa  Iguguno ambalo lina uwezo wa kuzalisha lita 135000 likiwa katika ukarabati baada ya kuanza kuvuja kwa ndani. Kazi hiyo inatarajiwa kukamilika muda wowote kuanzia sasa.

Mashine maalum ya kusukuma maji ya mradi wa iguguno ikiwa tayari kuanza kazi mara tu ukarabati wa matenki utakapokamilika.

Mhandisi wa Maji Wilaya ya Mkalama, Heke Bulugu (Kushoto)  akipokea maelekezo kutoka kwa mhandisi wa mradi huo Justin Kato (Mwenye shati jeupe).


Lile tatizo la ukosefu wa maji ya kutosha safi na salama katika baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Mkalama sasa limepatiwa ufumbuzi wa kudumu na muda si mrefu huduma hiyo muhimu itaanza kupatikana kwa maeneo yote ambayo hayakuwa na huduma hiyo.

Akimuongoza Mwenyekiti wa kamati ya huduma za jamii wa Wilaya ya Mkalama Bi. Mariam Kahola; Mhandisi wa Maji wa Wilaya ya Mkalama Heke Bulugu amesema kuwa kinachosubiriwa sasa ni fedha zilizobaki kwa ajili ya kumaliza kulipa madeni ya wakandarasi na baada ya hapo zoezi la umaliziaji wa miradi hiyo litafanyika.

“Jumatatu ya wiki ijayo nitakuwa Dar-es-salaam  kwa ajili ya kuzifuatilia pesa hizo na ntahakikisha pesa hizo zinapatikana haraka ili wananchi waanze kupata huduma hii ya maji kwa sababu msimu unaokuja wa kiangazi ndio huwa mgumu zaidi kwao” Alisema Bulugu.

Ziara hiyo ilihusisha miradi ya maji ya Gumanga, Nyahaa na ule wa Iguguno ambayo kwa pamoja inagharimu Zaidi ya bilioni moja kwa thamani ya pesa ya Tanzania.

“Natoa rai kwa watendaji na wenyeviti wa vijiji kuhakikisha wananchi hawafanyi shughuli za kilimo katika maeneo yaliyo karibu na miradi hiyo kwa sababu kufanya hivyo ni kosa kisheria” Alisisitiza Bulugu.

Alisema kuwa mwananchi yoyote atakayevunja sheria hiyo anapaswa kulipa faini ya shilingi Elfu hamsini pesa ambazo zinapaswa kuingia kwenye mifuko ya maendeleo ya vijiji ilipo miradi hiyo.


No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA