Monday 9 May 2016

AWAMU YA PILI YA UHAKIKI MKALAMA YAANZA LEO


Zoezi la uhakiki wa mara ya tatu  katika Mkoa wa Singida limeendelea tena leo ambapo timu ya wahakiki kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida imeanza kazi hiyo ya uhakiki wa kujiridhisha katika Wilaya ya Mkalama.

Uhakiki huo ambao unajumuisha kada zote za watumishi wa serikali kuu na wale wa serikali za mitaa unatarajiwa kufanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia leo ambapo unatarajiwa kufikia tamati siku ya Jumatano.

Mara baada ya kufika katika Ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, timu hiyo ya wahakiki ilikutana na wakuu wa idara na vitengo mbalimbali vilivyopo katika ofisi hiyo na kufanya kikao kifupi cha ufafanuzi na maelekezo chini ya Kaimu Mkurugenzi wa Wilaya hiyo,  Njelu Abdallah.

Akizungumza katika kikao hicho, mmoja wa  wahakiki hao Mbwana Mkingule alisema wahakikiwa wote wanapaswa kuwasilisha barua za ajira, barua za kuthibitishwa kazini na barua ya mwisho ya kupandishwa cheo kwa watumishi waliopandishwa madaraja yao.

“Kila mkuu wa idara anapaswa kuorodhesha majina ya watumishi wote waliopo chini ya idara yake na mwisho wa orodha hiyo kuwe na saini za Mkuu huyo huyo wa idara na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya” Aliongeza Mkingule

Aidha Afisa Utumishi wa Wilaya ya Mkalama, Pascal Lefi alipendekeza watumishi wa idara ya afya kuanza kuhakikiwa kutokana na unyeti wa idara hiyo kwa wananchi hivyo wanapaswa kuwahi kurejea kwenye vituo vyao vya kazi kuendelea kutoa huduma.

PICHA TATU CHINI ZIKIONESHA WATUMISHI WALIOJITOKEZA KATIKA SIKU YA KWANZA YA UHAKIKI WA WATUMISHI KATIKA OFISI ZA HALMASHAURI YA WILAYA YA MKALAMA LEO MAY 9, 2016.






No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA