PICHA 3 CHINI: SEHEMU YA VIFAA TIBA VILIVYOKABIDHIWA LEO.
Hamashauri ya Wilaya ya Mkalama leo imepiga hatua kubwa
katika sekta ya afya baada ya kupokea vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi
milioni 345,430,700.00 kutoka taasisi ya HumanBridge yenye makao yake makuu
nchini Sweden.
Miongoni mwa Vifaa hivyo ambavyo kwa niaba ya wananchi wa
Wilaya ya Mkalama vilikabidhiwa kwa Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Jackson Masaka
vinajumuisha Meza kwa ajili ya Upasuaji, Vifaa vya upasuaji, Magodoro 25,
Vitanda 25, Mashine ya kupima mapigo ya moyo, Vitanda vya kujifungulia kwa
wajawazito, Viti vya walemavu wa miguu, vifaa vya kusaidia kutembea kwa
wanaosumbuliwa na miguu na vingine vingi.
Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa vifaa hivyo, Mgeni
rasmi wa hafla hiyo ya mapokezi ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe.
Mhandisi Jackson Masaka aliishukuru taasisi hiyo hiyo kwa kuichagua Mkalama
kuwa Wilaya ya kwanza kupokea msaada wa aina hiyo ambapo aliwashukuru pia kwa
niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuunga mkono jitihada zake
za kuboresha sekta ya afya nchini.
“Alipoingia tu madarakani, Mhe. Rais Magufuli alianza na
sekta ya afya ambapo aliongeza wodi kwa ajili ya wanawake pale katika hospitali
ya Taifa ya Muhimbili hivyo kitendo hiki ni ishara pekee ya kuunga mkono
jitihada za Mhe. Rais” Alisema Mhe. Masaka.
Mhe. Masaka aliiomba taasisi hiyo kuendeleza ushirikiano
waliuoanzisha na Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ambapo aliwaahidi kutunza na
kusimamia matumizi ya vifaa tiba hivyo ili kuhakikisha wananchi wa Mkalama
wanafaidika ipasavyo na uwepo wa vifaa hivyo katika zahanati na vituo vyao vya
Afya pindi wakienda kutibiwa.
Akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mkurugenzi
wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga mbali na kuishukuru
taasisi hiyo, alisema kuwa vifaa hivyo vitamaliza mapungufu ya vifaa tiba yaliyokuwepo
katika zahanati na vituo vya Afya vilivyopo Wilayani hapa.
“Hata hii thamani ya vifaa iliyotajwa ni kwa mujibu wa
vile ambavyo vipo kwenye rejesta ya Bohari ya Dawa ya Taifa (MSD) lakini kuna vifaa vingine vingi ambavyo
tumeletewa hatujajua thamani yake kwa sababu havipo kwenye rejesta ya MSD hivyo
thamani ya vifaa tulivyokabidhiwa vinaweza kufika mpaka milioni 400” Alisema Sanga.
Sanga aliongeza kuwa vifaa hivyo vimefika katika
Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama katika wakati sahihi kwa sababu tayari
Halmashauri hiyo mbali na kuendelea na ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kinyambuli
hivi sasa, halmashauri hiyo katika bajeti ya mwaka wa fedha 2018/2019 imetenga
kiasi cha shilingi milioni 450 kwa ajili ya uboreshaji wa kituo cha Afya cha
Mkalama, Shilingi milioni 400 kwa ajili ya uboreshaji wa kituo cha Afya cha
Kinyangiri na shilingi milioni 100 kwa ajili ya ukamilishaji wa kituo cha Afya
cha Msiu.
Kwa upande wake muwakilishi wa taasisi ya HumanBridge
Mchungaji Bahati Kito alisema kuwa jitihada zilizooneshwa na viongozi wa Halmashauri
ya Wilaya ya Mkalama katika kuhakikisha vifaa hivyo vinatoka bandarini haraka
na kufika kwa walengwa zinapaswa kuigwa na Halmashauri nyingine kwani zimezidi
kuwashawishi kutoa misaada mingine zaidi.
“Moja ya Vitu ambavyo viliikatisha tamaa taasisi yetu
kutoa misaada mbalimbali nchini Tanzaniani suala la urasimu hasa baada ya
mizigo yetu kufika bandarini ambapo baadhi ya makontena tuliyotuma yaliishia
kuozea bandarini” Aliongeza Mchungaji Kito.
Mchungaji Kito alimalizia kwa kupongeza juhudi za dhati
zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe
Magufuli katika kulinda rasilimali za
Watanzania jambo ambalo linawapa moyo sana washirika wa nchi waliopo nje ya nchi.
No comments:
Post a Comment