Wednesday 23 March 2016

HARAMBEE YA MADAWATI MKALAMA YASHIKA KASI

 

Katika kuendelea kutekeleza maagizo ya Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzaniai aliyoyatoa kwa viongozi wote wa uma wakati akiingia madarakani, Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mh. Christopher Ngubiagai (Aliyesimama)ametangaza harambee inayotaraijiwa kufanyika Aprili 9,2016 kwa ajili ya kukusanya sehemu ya fedha itakayotumika kutengeneza madawati 6295.

Ngubiagai amesema ameamua kuchukua hatua hiyo ili kuhakikisha mpaka kufikia juni 30 mwaka huu hakuna mwanafunzi ambaye atakaa chini hasa ukizingatia kuwa serikali imeamua kutoa elimu ya msingi na sekondari bure hivyo ni lazima ihakikishe elimu hiyo inatolewa katika mazingira ya kuridhisha.

“Awali madawati yaliyokuwa yakihitajika ni 6773 lakini kuna wadau wametengeneza sehemu ya idadi hiyo na kubaki na idadi ya madawati 6295 ambayo gharama ya kuyatengeneza ni shilingi milioni 377 na laki 7 kwa mchanganuo wa shilingi elfu 60 kila dawati” Amesema Ngubiagai.

 Ametaja mikakati ambayo yeye kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama pamoja na watumishi wengine waliamua kuichukua ili kufikia malengo ya kukusanya kiasi hicho cha pesa au idadi hiyo ya madawati ambayo ni pamoja na Kufanya harambee itakayowashirikisha wadau wa elimu, wazawa  na wananchi wenye mapenzi na maendeleo ya Wilaya ya Mkalama kwa ujumla.
Ameongeza lengo la harambe hiyo ni kukusanya kiasi cha shilingi milioni 150  huku kiasi kingine cha pesa kilichobaki kikitarajiwa kukusanywa  kupitia pesa ya mfuko wa mbunge, baadhi ya taasisi ikiwemo benki ya NMB ambayo imeshakubali kuchangia sehemu ya madawati hayo, wananchi mbalimbali ambao wamehamasishwa kupitia mikutano ya vijiji na wadau wa sekta ya elimu.

Aidha amepongeza hatua ya watumishi wa halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kuahidi kuchangia sehemu ya idadi ya madawati hayo yaliyobakia ambapo ametoa rai kwa wadau wa Elimu na wananchi mbalimbali watakaoguswa na jambo hili kujitokeza kwa wingi siku ya harambee ili kuweza kuhakikisha hakuna mwanafunzi wa Wilaya ya Mkalama anayekaa chini ifikapo juni 30 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA