Saturday 27 October 2018

Mkalama inapiga hatua-Tulia

Naibu Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari Tulia Ackson akizungumza wakati wa harambee ya kuchangisha fedha za ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu wa wilaya ya Mkalama iliyofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya hiyo.

Mbunge wa viti maalum wa Mkoa wa Singida Mhe. Martha Mlata (kushoto) akimkabidhi zawadi ya mboga aina ya ''mnafu'' naibu spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dakatri Tulia Ackson wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu iliyofanyika leo kwenye ukumbi wa mikutano wa Halmashauri wilaya ya Mkalama.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhe. James Mkwega (kushoto)  akimkabidhi zawadi maalum spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari Tulia Ackson wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa Uwanja wa mpira wa miguu iliyofanyika leo kwenye ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya wilaya ya Mkalama

Naibu Spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (kulia) Mhe. Daktari Tulia Ackson akipokea jumla ya mifuko 100 ya saruji kutoka kwa Mbunge wa viti maalum Mhe. Martha Mlata (kushoto) huku tukio hilo likishuhudiwa na Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi Mhe. Lameck Itungi.




Naibu spika wa Bunge la  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari Tulia Ackson leo aliongoza viongozi na  mamia ya wananchi wa wilaya ya Mkalama katika harambee ya kuchangia ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu wa Wilaya hiyo.

Harambee hiyo ambayo mpaka kukamilika kwake ilifanikisha kupatikana jumla ya shilingi milioni 61 ilihusisha viongozi mbalimbali wa serikali, viongozi wa vyama vya siasa, wataalam mbalimbali wa Halmashauri ya wilaya ya Mkalama na wananchi kwa ujumla.

Wakati wa harambee hiyo Mhe. Tulia aliwasifu viongozi wote na watendaji wa wilaya ya Mkalama kwa jitihada mbalimbali wanazofanya katika kuhakikisha wilaya hiyo inapiga hatua kadri muda unavyokwenda.

“Najua Mkalama ni moja ya wilaya ambazo hazina muda mrefu sana tangu kuanzishwa kwake lakini nina uhakika kiwango chake cha maendeleo hivi sasa ni kikubwa kuliko baadhi ya Wilaya kongwe zilizoanzishwa muda mrefu hivyo niwapongeze sana kwa hilo” Alisisitiza Mhe. Tulia.

Baadhi ya viongozi waliohudhuria harambee hiyo na kutoa michango yao ni pamoja na Mbunge wa jimbo la Mkalama Mhe. Allan Kiula ambaye alichangia shilingi milioni 4, Mbunge wa viti maalum Mhe. Martha Mlata ambaye alichangia mifuko 150 ya saruji yenye thamani ya shilingi 2,250,000/= na Mbunge wa viti maalum Mhe. Asha-Rose Matembe ambaye alichangia mifuko 50 ya saruji.

Wengine waliochangia katika harambee hiyo ni pamoja na aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Mohamedi Mpinga ambaye alichangia mifuko 230 ya saruji, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mkalama ambayo ilitoa kiasi cha shilingi 550,000/=, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ambaye alichangia bati 98  na shilingi 500,000/=.

Mbali na viongozi hao wengine waliotoa au kuahidi michango yao kwenye harambee hiyo ni pamoja na wakuu wa idara wa Halmashauri ya wilaya ya Mkalama, waheshimiwa madiwani wa Halmashauri ya wilaya hiyo, wafanyabiashara mbalimbali waliopo ndani ya wilaya hiyo na wananchi mbalimbali waliopo ndani na nje ya wilaya hiyo.

Katika hafla hiyo, Mhe. Tulia alipewa rasmi jina la “Nzitu” ambalo asili yake ni kabila la wanyiramba likimaanisha mtoto ambapo mara baada ya kulipokea alimtangaza Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi wilaya ya Mkalama Mhe. Lameck Itungi kuwa baba yake rasmi wa kabila hilo.

  

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA