Friday 13 April 2018

TUTAIFUNGA IRAMBA KWAO-MKWEGA

Mbunge wa jimbo la Iramba Magharibi ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Daktari Mwigulu Nchemba akifunga goli la kwanza katika mchezo uliozikutanisha timu za Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama na wale wa halmashauri ya Wilaya ya Iramba uliochezwa jioni ya leo.

Mbunge wa jimbo la Iramba Magharibi ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Daktari Mwigulu Nchemba akitaka kumpita beki wa timu ya Wilaya ya Mkalama katika mchezo uliozikutanisha timu za Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama na wale wa halmashauri ya Wilaya ya Iramba uliochezwa jioni ya leo.


Wachezaji wa timu ya Madiwani ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama wakimsikiliza Kocha wao Bakari Ngoda (hayupo pichani) wakati wa mapumziko.

Mbunge wa jimbo la Iramba Magharibi ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Daktari Mwigulu Nchemba akishangilia na mashabiki wa timu yake mara baada ya mchezo uliozikutanisha timu za Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama na wale wa halmashauri ya Wilaya ya Iramba.


Mbunge wa jimbo la Iramba Magharibi ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Daktari Mwigulu Nchemba akipongezana na beki wa timu ya madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama John Tibu mara baada ya mchezo uliozikutanisha timu za Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama na wale wa halmashauri ya Wilaya ya Iramba.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhe. James Mkwega akizungumza machache muda mfupi kabla ya kumkaribisha Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Jackson Masaka jioni hii mara baada ya mchezo uliozikutanisha timu za Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama na wale wa halmashauri ya Wilaya ya Iramba.


Jioni ya leo katika Wilaya ya Mkalama imewekwa historia baada ya kuchezwa mchezo wa mpira wa Miguu kati ya timu ya Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama na timu ya madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba huku kikosi cha timu ya Iramba kikiongozwa na Waziri wa mambo ya ndani Mhe. Mwigulu Nchemba.

Katika Mchezo huo uliomalizika kwa timu ya Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kufungwa jumla ya magoli 3-1 kulikuwa na vivutio mbalimbali huku burudani kubwa ikiwa ni kiwango kizuri kilichokuwa kikioneshwa na Mhe. Nchemba na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga ambaye ndiye alikuwa mfungaji wa bao pekee la timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.

Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Iramba ilianza kuhesabu kalamu yake ya magoli kupitia kwa Mshambuliaji wake tishio katika mcheo wa leo Mhe. Mwigulu Nchemba ambaye alifunga goli hilo baada ya kuachia shuti kali kufuatia mpira uliompita beki wa timu ya Mkalama John Tibu.

Zikiwa zimesalia dakika chache kabla ya kuelekea mapumziko, Kiungo wa timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga aliisawazishia timu yake goli baada ya kukwamisha kiufundi wavuni penati yake iliyotokana na beki wa timu ya Iramba kuunawa mpira wakati akiwa kwenye heka heka za kuokoa mpira uliopigwa na Mshambuliaji Lunzegere Kilala.

Mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, timu hizo zilikuwa zimetoshana nguvu baada ya kutoka sare ya bao 1-1.

Maelekezo ya walimu wa timu zote mbili wakati wa mapumziko yalionekana kuzaa matunda zaidi upande wa timu ya Iramba baada ya kufanikiwa kupachika goli la pili kupitia kwa Mhe. Mwigulu Nchemba kwa mara nyingine tena huku safari hii akifunga goli hilo baada ya “piga nikupige” zilizotokea katika goli la timu ya Mkalama.

Mara baada ya kufungwa goli la 3 lililofungwa dakika 10 tu baada ya goli la pili, timu ya Mkalama ilifanya mabadiliko ya wachezaji hatua ambayo yalionesha mafanikio baada ya timu hiyo kuongeza kasi ya mashambulizi lakini hata hivyo kasi hiyo haikuweza kuzaa matunda kutokana na uhodari uliooneshwa na kipa wa timu ya Iramba ambaye alipangua michomo kadhaa iliyokuwa ikielekezwa golini kwake.

Mara baada ya kumalizika kwa Mchezo, Nyota wa mchezo huo ambaye pia ni  Mbunge wa jimbo la Iramba Magharibi Mhe. Mwigulu Nchemba aliushukuru Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kwa maandalizi mazuri ya tukio hilo huku akiomba jambo hilo liwe endelevu.

“Mimi na Mhe. Kiula tukiwa bungeni huwa tunashughulikia changamoto zetu kwa pamoja kwa sababu kwetu Iramba ni moja hivyo ni vizuri ushirikiano huu tuuenzi na kuudumisha” Aliongeza Mhe. Nchemba.

Akijibu ombi fupi lililowasilishwa na Mbunge wa jimbo la Mkalama Mhe. Allan Kiula kuhusu umaliziwaji wa kituo cha polisi kilichopo Nduguti, Mhe. Nchemba alisema kuwa katika bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani inayotarajiwa kusomwa tarehe 30  mwezi huu, kipaumbele cha Ujenzi na uboreshaji wa vituo vya polisi  kimewekwa Wilaya mpya zote ikiwemo Wilaya ya Mkalama.

“Lakini pia ombi la Mhe. Kiula la kutaka timu ya madiwani wa Halmashauri zote mbili za Iramba na Mkalama kucheza na timu ya bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepita hivyo tutakaa na Mhe. Kiula na kupanga tarehe rasmi ya mechi hiyo” Alisisitiza Mhe. Nchemba.

Mchezo huo ulitanguliwa na Mkutano wa baraza la madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama robo ya pili uliofanyika mapema asubuhi ambapo kamati mbalimbali ziliwasilisha taarifa zao na waheshimiwa madiwani kupata nafasi ya kuuliza maswali ya papo kwa hapo kwa Wenyeviti wa kamati hizo, Mkurugenzi na Wataalam mbalimbali wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.




No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA