Wednesday 20 September 2017

TEA ILIVYOBORESHA ELIMU MKALAMA

Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Bi. Sylvia Lupembe akipata maelezo kwa ufupi kutoka kwa mwakilishi wa Mkandarasi Mzinga Holding Cooperation kuhusiana na maendeleo ya ujenzi wa bweni na bwalo la Shule ya Msingi Munguli unaoendelea katika kitongoji cha Munguli

Mkadiriaji wa Ujenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Bi. Paskazia Tibalinda akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa bweni na bwalo la Shule ya Msingi Munguli unaoendelea katika kitongoji cha Munguli

Afisa Elimu Msingi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Chacha Kehogo akitoa maelezo machache kwa Meneja Mahusiano wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Bi. Sylvia Lupembe wakati wa ukaguzi wa ukaguzi wa ujenzi wa bweni na bwalo unaoendelea katika eneo hilo.

  

Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) Bi. Sylvia Lupembe (wa pili kutoka Kulia waliosimama) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanakijiji wa kijiji cha Munguli na wadau wa habari Muda mfupi kabla ya kumaliza ziara yake katika kijiji cha Munguli.



Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) ni chombo kilichosaidia kwa kiasi kikubwa sana kukuza na kuboresha kiwango cha Elimu nchini kwa kuwezesha miundombinu inayozunguka sekta hiyo nyeti kabisa  Ulimwenguni hivi sasa.

Katika Wilaya ya Mkalama, Mamlaka hiyo imewezesha kupatikana kwa miradi mikubwa miwili ambayo kwa namna moja au nyingine itasaidia kuinua kiwango cha udahili na ufaulu wa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.

Kitongoji cha Munguli ni eneo linapoishi kabila maarufu sana la Wahdzabe ambalo kwa miaka mingi tangu kupatikana kwa Uhuru limekuwa na mwitikio mdogo linapokuja suala la elimu hasa kutokana na kabila hilo kuishi mbali sana na mahali zinapopatikana huduma za kijamii.

Baada ya kuona changamoto hiyo Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kwa kushirikiana na TEA wameanza Ujenzi wa bweni na bwalo la chakula la kisasa kwa wanafunzi wa shule ya Msingi Munguli mradi ambao ukikamilika  utaongeza hamasa kwa jamii hiyo kushiriki katika haki yao ya Msingi ya kupata Elimu kwa kusaidia wanafunzi hao kuondokana na changamoto ya kutembea umbali mrefu mpaka kufika shuleni na pia itawahakikishia kupata huduma bora ya chakula kwa wakati hali itakayowawezesha  kupata muda mrefu zaidi wa kukaa shuleni.

Kwa mujibu wa Mkadiriaji wa  Ujenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Bi. Paskazia Tibalinda Mradi huo utagharimu kiasi cha shilingi milioni 184 kwa upande wa bweni na shilingi milioni 119 kwa upande wa bwalo na unatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miezi sita kuanzia sasa.

“Zoezi la uchimbaji wa msingi limechukua muda mrefu kidogo kutokana na uwepo wa mawe kwenye udongo wa eneo hili lakini tunashukuru tumemaliza na sasa kinachofuatia na kumwaga kifusi na jamvi ambapo baada ya hapo kazi hii itaanza kwenda kwa kasi” Aliongeza Bi. Tibalinda.

Akizungumza kwa niaba ya Mamlaka ya Elimu Tanzania wakati wa ziara ya ukaguzi wa mrad huo, Meneja Uhusiano wa Mamlaka hiyo Bi. Sylvia Lupembe ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kwa usimamizi mzuri wa mradi huo ambapo ametoa rai ya kukamilika kwa mradi huo kwa wakati na katika ubora ulioanza nao.

“Mradi huu ni maalum kwa sababu utaisaidia jamii maalum ya Watanzania kabila la wahadzabe  lakini pia utaibadilisha jamii hii kama ambavyo wenyewe wamesema kuwa wamekaa sana porini lakini hawatoacha Mila yao ila wanahitaji kupata elimu” Aliongeza Bi. Lupembe.

Bi. Lupembe ameiomba Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kuhakikisha kuwa mradi huo unakuwa chachu ya kuchochea maendeleo ya Elimu kwa kuongeza idadi ya udahili na ufaulu wa wanafunzi wa shule hiyo ambapo alisisitiza kuwa mamlaka hiyo itaendelea kufuatilia kwa ukaribu mpaka kukamilika kwa mradi huo.

“TEA tumefarijika sana kusikia Halmashauri imeshaanza kununua vitanda kwa ajili ya wanafunzi watakaoishi kwenye bweni hili pamoja na jengo kuwa katika hatua ya awali kabisa” Alimalizia Bi. Lupembe.

Akizungumza kwa niaba ya Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Afisa Elimu wa Wilaya ya Mkalama kwa upande wa shule za Msingi, Chacha Kehogo alisema kuwa halmashauri imejipanga vizuri kuupokea mradi huo mara utakapokamilika ambapo mpaka sasa tayari imeshanunua vitanda 31 ambavyo vimeshafika katika shule hiyo vikisubiri kukamilika kwa bweni.

“ Kwa hiyo niwahakikisheni TEA kuwa halmashauri ya Wilaya ya Mkalama itaendelea kuunga mkono jitihada mlizozionesha ili na sisi tuoneshe tunachoweza kufanya na hata  wadau wengine wakitaka kuja wasituone tegemezi hivyo niwashukuru sana na naomba msisite kututembelea tena kwa sababu bado tuna changamoto nyingi sana katka shule zetu hasa upande wa miundombinu. ” Alimalizia Kehogo

Mbali na mradi huo TEA imekamilisha ujenzi wa nyumba bora kabisa na ya kisasa ya walimu iliyopo katika kijiji cha Isanzu yenye thamani ya shilingi milioni 148  ambapo jumla ya Walimu tisa wa shule ya Sekondari ya Isanzu wanatarajia kuanza kuishi hapo muda wowote kuanzia sasa.

Ili uweze kumsikia na kumuona Meneja mahusiano wa TEA Bi. Sylvia Lupembe akizungumza katika ziara hiyo tafadhali bofya hapa

Ili uweze kumsikia na kumuona Afisa Elimu Msingi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Chacha Kehogo akizungumza katika ziara hiyo tafadhali bofya hapa


Ili uweze kumsikia na kumuona Mkadiriaji Majengo wa Halmshauri ya Wilaya ya Mkalama Bi. Paskazia Tibalinda akizungumza katika ziara hiyo tafadhali  bofya hapa

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA