Thursday 26 January 2017

SITAKI TENA KUSIKIA MSAMIATI "CHINI YA KIWANGO"- NCHIMBI

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi akizungumza na wakulima wa kijiji cha Nkungi juu ya umuhimu na faida za kilimo cha Viazi lishe kiuchumi na kiafya huku. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Jackson Masaka na kushoto kwake ni Afisa Kilimo wa Wilaya ya Mkalama ndugu Cuthbert Mwinuka.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi akianza shughuli ya kupanda viazi lishe katika shamba la kijiji cha Nkungi.

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Jackson Masaka akipanda viazi lishe katika shamba la kijiji cha Nkungi ili kuonesha ishara kuwa usalama wa chakula ni jukumu la kila mtu.

Katibu tawala wa Mkoa wa Singida Bi. Anjelina Lutambi akishiriki kwenye  zoezi la upandaji wa viazi lishe katika kijiji cha Nkungi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Injinia Geofrey Sanga akithibitisha kuwa usalama wa chakula ni jukumu la kila mtu wakati akipanda viazi lishe kwenye shamba la kijiji cha Nkungi.

Katibu tawala wa Mkoa wa Singida Bi. Anjelina Lutambi akishirikiana na mwanakijiji kuchimba mashimo ya kupandia viazi lishe katika Kijiji cha Nkungi jana.


Muuguzi wa Zahanati ya Nduguti na Mratibu wa damu salama Wilayani Mkalama Bi. Josephine Makanyaga akipokea zawadi kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi kama ishara ya kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa kuthamini mchango wake katika utoaji wa huduma ya Afya Wilayani hapa.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama (hawapo pichani) jana mchana.

Watumishi wa halmashauri ya Wilaya ya Mkalama wakimsikiliza kwa umakini Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi alipokuwa akizungumza nao mapema jana mchana.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe: Rehema Nchimbi au “mama Nchimbi” kama anavyojulikana Nchini jana aliendelea na ziara yake katika Wilaya ya Mkalama ambapo kabla ya kuzungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo alishiriki katika shughuli za kilimo kwenye vijiji vya Nkungi na Ilunda.

Tukio hilo la aina yake kuwahi kufanywa na viongozi wakuu wa serikali lilifanyika saa3 asubuhi ambapo mara tu baada ya kuzungumza na wananchi, Mhe: Nchimbi aliamuru viongozi wote waliofika katika ziara yake kijijini hapo akiwemo Katibu tawala wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya Mkalama, Katibu tawala wa Wilaya, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Mkalama, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Mkalama na wakuu wa idara washiriki katika kupanda zao la viazi lishe kwenye shamba lote la wanakijiji hao.
Mhe: Nchimbi alisema lengo la kufanya zoezi hilo ni kutoa elimu kwa wananchi kuwa jukumu la usalama wa  chakula si la Wananchi au wakulima pekee bali ni la Viongozi wote wanaowatumikia wananchi hao.

“Sipendi kiongozi anayesema yupo karibu na wananchi kwa sababu hatuwezi kupima ukaribu uliopo hivyo ni vyema kuanzia sasa tuache kuwa karibu na badala yake tuwe pamoja nao” Alisema Nchimbi.

Akiwa shambani hapo, Mhe: Nchimbi aliwataka viongozi wote na watumishi wa Wilaya kulima mazao ya viazi, mihogo au kufuga nyuki ili kuondokana na tabia ya kuilalamikia serikali kuwa mishahara inayowalipa haitoshi.

“Mwaka huu wa Kilimo Kila Mtumishi ni lazima awe na nusu heka ya Viazi au Mihogo au afuge nyuki mizinga miwili au afanye vyote kwa pamoja na baada ya miezi mitatu kuanzia sasa nitapita kukagua shughuli hizo” alisisitiza Nchimbi.

Akiwa kwenye Mkutano na watumishi wa halmashauri, Mhe: Nchimbi aliagiza kabla ya kusaini mkataba viongozi wote wa halmashauri ni lazima wakiri thamani ya mali zao zinazohamishika na zisizohamishika ili kama mradi utatekelezwa chini ya kiwango, mali zao zitumike kufidia pesa ya serikali iliyopotea.

“Mradi wakati unajengwa Mkurugenzi, Mwenyekiti wa halmashauri na wataalam wanauangalia bila kusema chochote, ukikamilika ndio wanakuambia umejengwa chini ya kiwango, kuanzia sasa sitaki kusikia msamiati wa ‘chini ya kiwango’.

Mhe: Nchimbi alimalizia kwa kuwaagiza wakuu wote wa shule za msingi na sekondari kuwaruhusu wanafunzi ambao wazazi wao hawana uwezo wa kushona sare za shule waendelee na masomo ili mradi taratibu nyingine wawe wamekamilisha.


“ Baada ya Elimu kuanza kutolewa bure, changamoto nyingine iliyobakia kwa baadhi ya wazazi ni uwezo wa kuwashonea watoto wao sare za shule, sasa ninaagiza wakuu wa shule za sekondari na Msingi wote Wilayani hapa kuwaruhusu watoto hao waingine madarasani hata kama hawajavaa sare za shule ili wasikose haki yao ya msingi kwa sababu ya sare tu”. Alimalizia Nchimbi.

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA