Monday 23 May 2016

MSIUZE ARDHI BILA KUFUATA UTARATIBU-NGUBIAGAI

Afisa tarafa ya Mwangeza Ndugu Edward Makala akitoa utambulisho mfupi wa serikali ya kijiji kwa Mkuu wa Wilaya Mkalama Mhe: Christopher Ngubiagai (aliyekaa)

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama, Ndugu Amon Sanga akitoa maelezo mafupi katika kikao cha kutafuta suluhu ya mgogoro wa Ardhi kilichofanyika katika eneo la Songambele, kijiji cha Hilamoto.

Kaimu Afisa Ardhi wa Wilaya, Imikigwe Mwanitu (aliyevaa fulana ya bluu) akisikiliza kwa makini maswali na kero za wanakijiji wa Hilamoto zinazohusiana na Ardhi.

Wanawake wa jamii ya kimang'ati ambao pia ni sehemu ya jamii ya wakazi wa kijiji cha Hilamoto wakimsikiliza kwa umakini Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Christopher Ngubiagai (hayupo pichani).

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Christopher Ngubiagai akiwahutubia wananchi wa kijiji cha Hilamoto kuhusiana na kero zao za masuala ya ardhi alipofanya ziara wikiendi iliyopita.

Wananchi wa Kijiji cha Hilamoto wakiwa wamekaa kuuzunguka mti wa Mgungamaji maarufu kijijini hapo kama "mti wa amani" huku wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Christopher Ngubiagai aliyesimama katikati. Mgungamaji  ndio mti uliotumika kutengenezea madawati katika tarafa yote ya Mwangeza.

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe: Christopher Ngubiagai amewataka kutouza maeneo wanayomiliki kinyemela bila kupata ushauri kutoka kwa wataalam kwa sababu jambo hilo ndio linalozalisha migogoro mikubwa ya ardhi iliyopo hivi sasa.

Ngubiagai aliyasema hayo alipoenda katika kijiji cha Hilamoto kilichopo Wilayani hapa ambako kuna mgogoro wa ardhi kati ya Wanakijiji wa Hilamoto na mwekezaji anayefahamika kwa jina la Eugine Afrika.

Katika mgogoro huo wanakijiji wa Hilamoto wanamtuhumu mwekezaji huyo kumiliki ekari 500 za Kijiji hicho bila makubaliano yoyote na wanakijiji hao na badala yake aliwasilisha hati ya mahakama inayowataka wanakijiji hao kumpa Afrika kiasi hicho cha Ardhi.

“Niliagiza huyo Mwekezaji alete nyaraka zinazozibitisha umiliki wake wa hiyo ardhi lakini badala yake nikaletewa nakala ya hukumu ambayo inaonesha alishinda kesi iliyofunguliwa kupinga umiliki wa ardhi hiyo hivyo nilishindwa kuchukua hatua yoyote kwa sababu siwezi kuingilia au kupinga maamuzi ya mhimili wa mahakama” Alisema Ngubiagai.

Badala yake, Ngubiagai aliwashauri wanakijiji hao kuwasiliana na ofisi ya Mwanasheria wa Wilaya ili aweze kuwashauri namna ya kulishughulikia suala hilo jambo hilo lifanyike kupitia muhtasari kamili wa mkutano wa kijiji hicho.

Aidha Ngubiagai aliwatahadharisha wanakijiji hao kuhakikisha kuwa hakukuwa na namna yoyote ya uuzaji wa ardhi hiyo ili kupata nguvu ya malalamiko yao vinginevyo jitihada hizo hazitazaa matunda yoyote na badala yake wanakijiji hao watapoteza pesa na muda wao.

“Kumekuwa  na utaratibu wa wanakijiji kuuza maeneo wanayomiliki bila kufuata utaratibu wowote, matokeo yake wakiona yule waliyemuuzia anatengeneza faida kubwa kupitia maeneo hayo wanaanza kulalamika kuwa wamedhulumiwa maeneo yao, tabia hiyo muache mara moja” Aliongeza Ngubiagai.

Kuhusiana na mgogoro wa mpaka wa Mlima Dominiki unaohusisha Wilaya ya Mkalama na Mbulu, Ngubiagai alisema kuwa amemuandikia barua Mkuu wa Wilaya Mbulu ili waweze kukaa kikao cha ujirani mwema na kuzungumza kuhusiana na hilo lakini bado hajapata majibu ya barua hiyo lakini amemuandikia barua nyingine hivyo anasubiri majibu.



3 comments:

  1. Hahahahaha, Naona Kaimu Afisa Ardhi katika umakini mkubwa... All in all keep up a good work son.. SALUTE

    ReplyDelete

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA