Friday 22 April 2016

NITAENDELEA KUTUMBUA MAJIPU- NGUBIAGAI

Mkuu wa Wilaya ya Mkalama ambaye pia ni Kaimu mkuu wa Wilaya ya Iramba Mheshimiwa Christopher Ngubiagai amesema kuwa kasi yake ya kuwasimamisha watendaji wazembe itaendelea mpaka pale watumishi katika Wilaya hizo watakapofuata maadili ya kazi zao.

Ngubiagai ameyasema hayo kufuatia baadhi ya watumishi wa Wilaya ya Iramba kutamka wazi kuwa hivi sasa hali katika halmashauri hiyo imebadilika kabisa na kila mtu amekuwa akifanya kazi kwa kuogopa kusimamishwa kazi pindi akikosea.

“Kama unafanya kazi zako vizuri na unatimiza wajibu wako vizuri sitokuwa na tatizo na wewe kabisa lakini wale wazembe na wabadhirifu wote nitaendelea kuwasimamisha na kama wakipatikana na hatia nitawakabidhi kwenye mkono wa sheria”.

Alisisitiza wale wote wanaowafahamu watu wanaokiuka maadili ya kazi kwa kushiriki vitendo vya kifisadi wawapo ofisini, wasisite kutoa taarifa ili kuepuka kuwaonea watu wasio na hatia.

“Kuna hili suala la ubadhirifu wa zaidi ya milioni mia tano za lile jengo la Zahanati pale ambalo bado halijakamilika, Nitakuja kwa ajili ya kufuatilia na kushughulika na wale wote ambao wamehusika katika ufisadi wa ujenzi ule”

Katika kuunga mkono jitihada zinazooneshwa na Watendaji wa serikali yake, Jana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliwajibu wale wote wanaobeza staili yake ya kutumbua majipu na kusema kuwa mtu aliyeiba hadharani anapaswa kufukuzwa hadharani pia.

No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA