Monday 10 September 2018

Nataka daraja likamilike mwezi machi-Magufuli



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari John Pombe Magufuli akikata utepe kuashiria tukio la uwekaji wa jiwe la msingi la daraja la mto Sibiti mapema leo huku akishuhudiwa na viongozi mbalimbali wa serikali.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari John Pombe Magufuli akiwaongoza viongozi mbalimbali zoezi la uwekaji jiwe la msingi  la daraja la mto Sibiti mapema leo. 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari John Pombe Magufuli akiwaaga wananchi waliojitokeza kwenye hafla ya uwekaji jiwe la msingi daraja la Sibiti mapema leo.

Baadhi ya waheshimiwa madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama wakiwa kwenye hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la daraja la Mto Sibiti mapema leo tukio lililofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari John Pombe Magufuli.

Sehemu ya umati wa watu uliojitokeza kwenye hafla ya uwekaji jiwe la msingi la daraja la mto Sibiti  iliyofanyika mapema leo darajani hapo.


“Haiwezekani  ujenzi wa daraja uchukue zaidi ya miaka sita wakati mkandarasi analipwa stahiki zake zote kwa wakati tena kwa kutumia kodi za Watanzania hivyo daraja hili ni lazima likamilike ifikapo mwezi machi mwakani, Wizara mjipange kweli kweli kwa sababu tutafukuzana hapa hapa na kuanzia sasa hivi nalifanya kuwa kipaumbele changu namba moja kwa kulifuatilia hivyo ntapiga simu usiku na mchana ili kujua limefikia wapi”

Ni kauli iliyotolewa mapema leo na Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daktari John Pombe Magufuli wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la Msingi la Mto Sibiti baada ya kutofurahishwa na kasi ya mkandarasi anayejenga daraja la mto huo  huku pia akizikataa sababu mbalimbali za uchelewaji huo zilizotolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa wakala wa barabara wa Taifa (TANROADS) Mhandisi Patrick Mfugale na Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Mhe. Isack Kamwelwe.

“Waziri kama unaona mkandarasi huyu hana uwezo wa kumaliza kazi hii kwa wakati ni bora utafute mkandarasi mwingine kwa sababu sina uhakika hata kama mkandarasi huyu ana vifaa vya kutosha kumaliza kazi hii na huenda hata hivi navyoviona hapa vimeletwa jana usiku baada ya kusikia ninakuja leo” Aliongeza Mhe. Magufuli.
Mhe. Magufuli aliwaagiza wenyeviti wa bodi ya wakandarasi na washauri wa wakandarasi kuwasimamia ipasavyo mkandarasi na mshauri wa mkandarasi  wa daraja hilo na kama wataonekana kufanya kazi chini ya kiwango wachukuliwe hatua kwa mujibu wa taratibu za bosi hizo.

“Nyie ‘consultants’  mnapaswa kujua mpo hapo kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na najua nyie ni wafanyabiashara but this is not a good business for you  so watch out’’ Alionya Mhe. Magufuli.

Katika hotuba yake Mhe. Magufuli aliieleza halaiki ya wananchi waliojitokeza katika tukio hilo kuwa baada ya kukamilika kwa daraja hilo  uchumi wa Mikoa ya Singida na Simiyu utaimarika zaidi kwa sababu utawapa fursa wananchi wa pande hizo mbili kufanya biashara ya rasilimali wanazozalisha.

“Waziri wa Madini amesema hapa kuwa Mkoa wa Simiyu una chumvi nyingi sana kwa hiyo nategemea kukamilika kwa daraja hili kutachochea uchimbaji zaidi wa chumvi hiyo ambapo kiwango kikiridhisha tunaweza hata kuongeza kodi ya uingizaji wa chumvi ya nje ili kuongeza matumizi ya chumvi tunayozalisha wenyewe hapa ndani” Alisisitiza Mhe. Magufuli.

Mhe. Rais alihitimisha hotuba yake kwa kumpongeza Mbunge wa Mkalama Mhe. Allan Kiula kwa ushirikiano mzuri alionao dhidi ya wanasiasa wenzake ndani ya Wilaya na wataalam wote wa Wilaya hiyo ambapo alimtaka kuendeleza ushirikiano huo ili kuzidi kuongeza maendeleo ya Wilaya hiyo.

Awali akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Daktari Rehema Nchimbi alimshukuru Mhe. Magufuli kwa ujenzi wa daraja hilo ambapo alimhakikishia kuwa tayari Mkoa wa Singida umejipanga kuhusu matumizi sahihi ya daraja hilo na mkakati wa utunzaji wa mazingira yanazunguka daraja hilo umeshakamilika.

“Mhe. Rais ninakushukuru kwa sababu hivi sasa maji ya ziwa Victoria yatakayopita Simiyu yatafika mpaka Singida kupitia Mkalama” Alisema Mhe. Nchimbi.

Mpaka sasa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetumia zaidi ya shilingi bilioni 2002 za mapato yake ya ndani katika kuboresha na kutengeneza miundombinu ya barabara huku daraja la Sibiti likigharimu jumla ya shilingi bilioni 16 mpaka kukamilika kwake ambapo kwa sasa limefikia asilimia 70 na kugharimu shingi bilioni 15.








No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA