Mkoa wa Singida kupitia Wilaya ya Mkalama na mkoa wa
Manyara kupitia wilaya ya Mbulu leo wameadhimisha tamasha la pamoja la
utamaduni wa makabila makuu yaliyopo kwenye mikoa hiyo tukio lililofanyika
katika kijiji cha Hydorm.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa ni Katibu Mkuu
wa Wizara ya Habari, Sanaa utamaduni na Michezo Bi. Suzan Mlawi ambaye
alizipongeza wilaya hizo kwa kufanikisha maadhimisho ya tamasha hilo huku
akisisitiza kuwa suala la kudumisha mila na utamaduni wa watanzania ni jukumu
la kila mwananchi.
“Mwalimu Nyerere aliwahi kusema Taifa lisilo na utamaduni
ni sawa na taifa lililokufa hivyo ni lazima kila mmoja wetu aenzi na kudumisha
mila na desturi zetu kwani ndio kitambulisho chetu hata tunapokuwa nje ya nchi
yetu” Alisisitiza Bi. Mlawi.
Bi Mlawi aliongeza kuwa maadhimisho hayo ni ishara kubwa
inayoonesha ushirikiano wa dhati uliopo baina ya Wilaya ya Mkalama na Mbulu
ambapo aliwasihi viongozi wa pande hizo mbili kuendeleza na kudumisha umoja huo
huku wakiendelea kuenzi mila na desturi za Mtanzania.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi
Jackson Masaka aliipongeza kamati ya maandalizi ya tamasha hilo na kuwataka
wananchi wote wa Wilaya ya Mkalama kuhakikisha wanajitokeza kwenye tamasha hilo
ambalo litafanyika kila mwaka.
“Kuhudhuria tamasha hili ni utalii tosha kabisa na mtu
anaweza kuja na familia yake kwa ajili ya mapumziko hivyo nawasihi wananchi wa
Mkalama na maeneo mengine ya jirani wafike kushuhudia tukio hili la asili
kabisa” Alisisitiza Mhe. Masaka.
Tamasha hilo lilipambwa na burudani mbalimbali za asili
kutoka makabila ya Wagogo, Wasukuma, Wangoni, Wahadzabe, Wanyiramba, Wanyisanzu, Wairaqi, Wamasai na Wadatoga huku kivutio
kikubwa kikiwa ni vipaji vilivyooneshwa na mbunge wa jimbo la Mbulu
vijijini Mhe. Flatei Massay na Mkuu wa
Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka ambao walionesha ustadi mkubwa
katika kucheza ngoma na nyimbo za asili.
Mbali na ngoma na nyimbo za asili kutoka katika makabila
tofauti, tamasha hilo lilijumuisha pia maonesho ya vitu mbalimbali vya asili,
wanyamapori kama vile Simba, Chui, Mamba na kobe mwenye umri wa miaka 200 na
utamaduni wa kabila la Wadatoga.
Kijiji cha Hydorm kilichopo mpakani mwa Wilaya ya Mkalama
na Mbulu kwa sasa kinatambulika kama kitovu cha Afrika kutokana na kujumuisha
makundi makuu manne ya jamii za bara la Afrika ambao ni Wanyiramba na
Wanyisanzu (Wabantu), Wadatoga (Wanailo), Wahadzabe (Wakwesa) na Wairaqi
(Wakushi).
Miongoni mwa wadhamini wakubwa wa tamasha hilo kwa mwaka
huu ni pamoja na serikali ya Norway
chini ya kitengo cha Utamaduni kinachojulikana kama 4CCP (4 Corners Cultural
Programs), Mbuga ya wanyama ya Ngorongoro, Kampuni ya Yara, Shirika la bima ya
afya la MHI na benki ya CRDB.
No comments:
Post a Comment