Monday 13 June 2016

TASAF YAWA MKOMBOZI MKALAMA


Bi Emeliana Mkoma ambaye ni moja wa walengwa wa Tasaf alipotembelewa nyumbani kwake jana. Picha Chini ndio nyumba aliyojenga kwa ruzuku ya Tasaf.


Bi Leah Mpinga akiwa anazungumza na ujumbe wa Tasaf mara baada ya kufika nyumbani kwake jana. Picha Chini ni Mbuzi aliowanunua kutokana na ruzuku ya Tasaf.


Hivi sasa Wankembeta Kingu hawezi tena kufuata ruzuku bali humtumia mlezi wake wa nyumbani lakini kila anapopata ruzuku hiyo hutumia katika shughuli za maendeleo kama unavyoshuhudia picha mbili chini mavuno ya maharagwe aliyopata mara baada ya kuvuna msimu huu.




Maisha ya Bertha kingu kabla ya kuingizwa kwenye mpango wa Tasaf yalikuwa ni ya kuhama hama hasa baada ya nyumba yake kuanguka lakini kupitia ruzuku ya Tasaf amefanikiwa kujenga nyumba yake na kushiriki kikamilifu kwenye kilimo na kuvuna akiba ya kumtosha kabisa kama unavyoshuhudia katika picha mbili chini.



Mailungu Kingu alivunjika kiuno chake miaka kadhaa iliyopita hali iliyomlazimu muda wote kukaa au kulala tu. Lakini Mfuko wa Mendeleo ya Jamii Nchini (TASAF) wilaya ya Mkalama umemfanya kuwa mwenye matumaini muda wote kwani ameweza kununua kondoo na kuezeka nyumba yake kwa bati kama unavyoishuhudia katika picha chini.


Mlengwa Bi Wampumblya Joseph akiwa na mwanae alipotembelewa na Ujumbe wa Tasaf Wilaya ya Mkalama jana.

Hii ndio nyumba aliyokuwa akiishi Bi Wampumblya Joseph kabla ya kuingizwa kwenye mpango wa Tasaf.

Na hii ndio nyumba aliyofanikiwa kujenga kupitia ruzuku anazopata kutoka Tasaf.

Mfuko wa Mendeleo ya Jamii (TASAF) Wilayani Mkalama umeendelea kuziwezesha kaya masikini ili kujikwamua kutoka katika hali waliyo nayo.

Mapema kabla ya kuwawezesha wananchi wa vijiji vya Iambi na Mwando, Ofisi ya Mfuko huo Wilayani Mkalama ilifanya tathmini ya kutambua na kuangalia shughuli mbalimbali walizofanya baadhi ya walengwa kutokana na ruzuku walizopewa awamu iliyopita.

Emiliana Mkoma ni mmoja wa walengwa wa Mradi huo kutoka kijiji cha Mwando ambaye anasema kuwa mradi huo umemuwezesha kununua Mbuzi watatu, Mabati sita ya kuezeka nyumba yake hali iliyomuondoa kwenye nyumba ya tembe ambayo ilikuwa ikihatarisha maisha ya familia yake hasa msimu wa mvua.

“Lakini pia ruzuku ya Tasaf imeniwezesha kuwasomesha watoto wangu wawili ambao sikuwa na uhakika wa kuwaendeleza kimasomo hasa baada ya kifo cha baba yao lakini namshukuru Mungu hivi sasa mmoja amemaliza darasa la saba na mwingine amemaliza kidato cha nne, Hiyo yote imetokana na mchango mkubwa wa Tasaf” Aliongeza Emiliana.
Mlengwa wa Pili alikuwa ni Leah Mpinga ambaye kutokana na umri mkubwa alionao na maradhi yaliyokuwa yakimuandama mara kwa mara ilimuwia vigumu kuweza kujihudumia lakini mara baada ya Tasaf kuanza kumuwezesha amerejewa na matumaini na uhakika wa kupata huduma zote za msingi anazohitaji.

“Nimefanikiwa kuutibu mguu wangu ambao ulikuwa unakaribia kukatwa kutokana na maumivu makubwa niliyokuwa nayapata na jambo la pili nimefanikiwa kununua Mbuzi ambao wanaendelea kuzaa hivyo nategemea kuwa na mbuzi wengi sana siku za usoni” Aliongeza Bi. Mpinga.

Kwa upande wake bi Wankembeta Kingu ambaye kwa sasa amezeeka sana kiasi cha kuchukuliwa ruzuku na msimamizi wake pale anapoishi, aliishukuru serikali kupitia Tasaf kwa kumuwezesha kupata matibabu kwa urahisi pindi alipolazwa na kununua mbuzi wawili ambao anatarajia wazae ili awauze siku zijazo.

“Pia natumia ruzuku nazopewa kwenye kilimo hasa kwenye manunuzi ya mbegu na mbolea na mavuno ndo kama unavyoyaona hapo, alisema Bi Kingu huku akielekeza kidole kwenye viroba vikubwa vilivyojaa maharagwe yaliyovunwa.

Bi Nzitu Shilla ni miongoni mwa wanufaikaji hao wa mfuko wa Tasaf Wilaya ya Mkalama ambapo alikiri jambo kubwa alilofanya kupitia ruzuku aliyokuwa akipewa ni ujenzi wa nyumba anayoishi ambapo alifanikiwa kununua mabati na kufyatua matofali ya udongo imara ili kuwa na uhakika wa kutopata madhara kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa hasa msimu wa upepo mkali na Mvua.

Tasaf Mkalama ilizidi kuchanja mbuga ili kujionea kwa macho yao wenyewe matumizi ya ruzuku ambazo wamekuwa wakitoa ambapo safari hii walibisha hodi nyumbani kwa Bertha Kingu ambaye kabla ya kuanza kupata ruzuku alikuwa akiishi katika nyumba za watu kutokana na nyumba yake ya awali kuanguka baada ya kutokuwa imara.

“Nilipata manyanyaso sana kutoka kwa wenye nyumba hali ambayo kuna muda ilinilazimu nikose mpaka hamu ya kula kwani muda wote nilikuwa nawaza nyumba ya kuhamia mara baada ya kufukuzwa lakini nashukuru nilipoingizwa kwenye huu mpango wa ruzuku wa Tasaf nimefanikiwa kujenga nyumba yangu,ninafuga kuku na nimefanikiwa kulima mahindi na kupata mavuno ya kunitosha” Alisema Bertha.


No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA