Thursday 8 March 2018

MKALAMA YAADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA WANAWAKE

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida Mhe. Asha-Rose Matembe akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya kimataifa ya Wanawake iliyoadhimishwa leo katika kijiji cha Mwando Wilayani Mkalama

Diwani wa Viti Maalum kata ya Iguguno Mhe.Mariam Kahola (kushoto), Katibu wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha mapinduzi Wilayani Mkalama Bi. Fatma Ndee (katikati), Kaimu Afisa Elimu Msingi Bi. Rose Kibakaya na wengine pichani wakicheza muziki wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya wanawake yaliofanyika leo katika Kijiji cha Mwando Wilayani Mkalama.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya kimataifa ya Wanawake iliyoadhimishwa leo katika kijiji cha Mwando Wilayani hapa.


Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka  akitoa hotuba katika maadhimisho ya Siku ya kimataifa ya Wanawake iliyoadhimishwa leo katika kijiji cha Mwando Wilayani hapa.


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhe. James Mkwega akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya kimataifa ya Wanawake iliyoadhimishwa leo katika kijiji cha Mwando Wilayani hapa.

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida Mhe. Asha-Rose Matembe akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Mkalama na Viongozi wengine wa Wilaya hiyo Mifuko 30 ya Saruji ikiwa ni sehemu ya ahadi yake ya Mifuko 50 ya Ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Mwando, Zoezi hilo limefanyika leo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya wanawake iliyoadhimishwa Kiwilaya Kijijini hapo.

Wilaya ya Mkalama leo imeungana na maeneo mengine yote kusherehekea siku ya kimataifa ya wanawake iliyofanyika katika kijiji cha Mwando  yakiwa ni maadhimisho ya tano ya sikukuu hiyo tangu kuanzishwa kwa Wilaya hii.

Katika maadhimisho hayo ambayo mwaka huu yamebebwa  na kauli mbiu ya kitaifa isemayo “Kuelekea Uchumi wa Viwanda tuimarishe usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa Wanawake” viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Mkalama na Mkoa wa Singida kwa ujumla walitumia fursa hiyo kuhamasisha wanawake kujitokeza katika fursa mbalimbali na kupiga vita hali ya utegemezi dhidi ya wanaume.

Mbunge wa Viti maalum Mkoa wa Singida Mhe. Asha-Rose Matembe aliwaasa wanawake wote Wilayani Mkalama kujunga kwenye Vikundi ili waweze kukidhi vigezo vya kupatiwa mikopo ya Serikali na taasisi mbalimbali za fedha.

“Niwaombe Sido na taasisi mbalimbali za fedha watembelee vikundi vya wanawake na kutoa elimu ya Ujasiriamali ili fedha wanazokopeshwa ziweze kuwa na tija” Alisisitiza Mhe. Matembe.

Mhe. Matembe pia amepongeza jitihada za wazi zilizooneshwa na wananchi wa Kijiji cha Mwando kwa Kujenga Zahanati ambapo aliunga mkono jitihada hizo kwa kuwaahidi kuchangia mifuko 50 ya Saruji huku 30 akiikabidhi hapo hapo na mingine 20 kuahidi kuitoa ndani ya siku chache zijazo.

Awali kabla ya Kumkaribisha Mgeni Rasmi wa maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama Mhandisi Godfrey Sanga aliainisha jitihada mbalimbali ambazo serikali imezifanya ndani ya Wilaya ya Mkalama katika kuinua Ustawi wa wanawake ambapo mbali na Asilimia 5 inayokwenda kwenye vikundi vya wanawake vilivyosajiliwa kila Mwezi, Serikali pia inatarajia kukamilisha wodi ya wanawake iliyopo  katika Zahanati ya Nduguti ndani ya Siku 60 kuanzia sasa.

“Pia ndani ya Miezi miwili ijayo tunatarajia kukamilisha Ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kinyambuli ambacho ndani yake kuna Chumba kikubwa cha Upasuaji kwa wanawake wajawazito jambo ambalo litazidi kuhakikisha usalama wa afya za wanawake waliopo Wilayani Mkalama” Alisisitiza Sanga.

Sanga aliongeza  kuwa Bweni la Wanafunzi wa kike katika Shule ya Sekondari Nduguti linatarajiwa kukamilika muda wowote kuanzia hivi sasa hivyo kuanzia Muhula ujao wanafunzi wa Kike wote waliopo shuleni hapo watakuwa wakiishi bwenini jambo litakaloongeza usalama wa watoto wa kike pindi wakiwa shule.

Katika hotuba yake, Mgeni rasmi wa maadhimisho hayo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Mkalama Mhe. Mhandisi Jackson Masaka ameainisha aina mbalimbali za Unyanyasaji wa wanawake unaoendelea katika jamii likiwemo suala la ndugu wa Marehemu kuchukua Mali pindi mwanamke anapofiwa na mumewe.

“Jambo hili katika Wilaya ya Mkalama sitaki kulisikia na naagiza hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi ya watakaobainika kufanya hivyo” Aliongeza Mhe.Masaka.

Mhe. Masaka aliongeza kuwa kumekuwa na tabia isiyopendeza kwa baadhi ya wanaume ambapo wamekuwa wakiwalaumu wake zao pindi watoto wanapoharibikiwa kimaadili huku wakisahau kuwa jukumu la malezi ya watoto ni la baba na mama kwa pamoja na si mama peke yake.

“Lakini bado kuna baadhi ya kaya ambazo mpaka leo hazimpi mwanamke haki ya kupanga uzazi na bado jamii imekuwa ikifumbia macho badala ya kutoa ushauri unaofaa jambo ambalo linasababisha wanawake kuchoka sana kwa kuzaa mfululizo bila kufuata uzazi wa mpango” Alisema Mhe. Masaka.

Mhe. Masaka alihitimisha hotuba yake kwa kuwataka wanawake wote Wilayani Mkalama kutoona ni jambo la kawaida kwa watoto wao wa kike kupata ujauzito wakiwa shuleni kwa sababu takwimu zinaonesha kiwango cha watoto wa kike wanaopata ujauzito wakiwa Shuleni ni asilimia moja tu hivyo ni lazima wazazi wa watoto hao waungane na hiyo asilimia 99 ili kutokomeza kabisa hali hiyo.

“Mpaka sasa Jumla ya Kesi tatu za ubakaji zimeshafikishwa Mahakamani Wilayani hapa na wahusika wote waliokutwa na hatia wamehukumiwa vifungo” Alimalizia Mhe. Masaka.





No comments:

Post a Comment

HALMASHAURI YA WILAYA MKALAMA